Bukobawadau

KARAGWE YA SASA NA YA KITAMBO HAPO ZAMANI……WANYAMBO, KAHAWA, WAKIMBIZI, PESA, JIMTEX, JIE FANG, LAND ROVER 109!

 Zao la kahawa nguzo kubwa kwa wananchi wa Karagwe,bukobawadau blog tunatumia fursa hii kuwakumbuka wazee wetu wapambanaji  akina mzee Girigoli na Wenzake,Simoni Gabagambi,Chipukizi bus services na wengineo...
Mpaka hivi leo Wilaya yaKaragwe haijawahi kuishiwa utajiri wa mali (Kahawa, Ng'ombe, Mbuzi, Kondoo, Ndizi, Viazi, n.k)
 Miaka ya kati ya tisini kwenda mpaka mwanzoni mwa 2000, Kahawa ilistawi sana Karagwe na bei ya Kahawa-maganda ilikuwa nzuri sana. Ni kipindi hiki hiki pia machafuko katika nchi za jirani hasa Rwanda yalikuwa yameshika kasi na kusababisha wakimbizi wengi kuingia Karagwe. Mambo haya yalizidi kushamirisha mazingira ya Biashara wilayani Karagwe. Mashirika ya Kimataifa yaliingia kwa kasi, mahitaji ya huduma yakapanuka na hivyo kupanua Biashara.

Wanyambo siku zote ni matajiri wa mali (ng’ombe, ndizi, kahawa, n.k) lakini katika kipindi hiki waliukwaa utajiri wa maburungutu ya fedha na wasijue jinsi ya kuyawekeza! Kila aliyepata hela akajikuta ananua lori la kichina “JIE FANG” wao wanatamka (EJIIFWONGO) au Land Rover 109. Walioishia kununua Land Rover kauli mbiu yao ilikuwa “walau ipaki (gari ) kwenye uwanja wangu” (Buzima njipaki omuchibuga). Zilinunuliwa “JIE FANG” kwa wingi mpaka Wakala wa hii Kampuni, Ukanda wa Afrika ikambidi kutembelea hiyo nchi inayoitwa “Karagwe”. Wanyambo walikuwa wanakwenda Dar kununua haya magari wakiwa wamebeba pesa taslimu! Mtihani wao mkubwa ulikuwa sehemu kuu mbili; kupita pori la Kitengure na jinsi ya kufika Kastamu baada ya kushuka kwenye gari pale stendi.

Vibaka wa Bukoba walikwisha soma jinsi gani Wanyambo wenye hela hupenda kuvaa na huzificha wapi. Enzi hizo matajiri hawa waliamini kuvaa kikawaida au hovyo hovyo ni njia sahihi yenye usalama unapokuwa na pesa. Na sijui kama ilikuwa kwa bahati mbaya, lakini wengi wa walioshindwa kuvuka Bukoba, yaani walioibiwa hela mjini walipendelea kuvaa jaketi za BMW na hela walizihifadhi kwenye mikoba ya ngozi iliyofahamika zaidi kama JIMTEX. Kwa hiyo siku za meli (Jumatatu, Jumatano na Ijumaa) vibaka walikuwa wakiona “AKA-JIMTEX” wanafuatilia kwa Karibu. Eneo mbele ya soko kuu mpaka zilipokuwa Bucha za Kaloleni (usawa wa Cosmopolitani) wamelizwa Wanyambo wengi sana.

Leo hii ukitembelea Karagwe vijijini maeneo kama Kaisho, Kabirizi, Kyelwa, Nkwenda, Katembe, Mulongo utakuta malori mengi sana ya JIE FANG mabovu yamepaki. Pia utaona Land Rover 109 na kuhadithiwa kwamba nyingi hazikutembea hata kilometa moja baada ya kununuliwa na kufikishwa nyumbani.

Marejeo haya ni kwa hisani ya Mc Baraka Galiatano Owner & founder http://bukobawadau.blogspot.com/

 Muonekano wa Mji wa Kamachumu
Muonekano wa sasa kijiji cha Buganguzi
Next Post Previous Post
Bukobawadau