Bukobawadau

CHADEMA SASA WAWAGEUKIA POLISI

Dar es Salaam.Tukio la Mwenyekiti wa Chadema Wilaya ya Temeke, Joseph Yona kutekwa nyara, kupigwa na kutupwa katika vichaka eneo la Tegeta na watu aliodai kuwa ni wafuasi wa chama hicho, limekichanganya Chadema baada ya jana kudai kuwa tukio hilo limefanywa na Jeshi la Polisi.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Katibu wa Chadema Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Henry Kilewo alitolea mfano matukio kadhaa yaliyowakuta wanachama wa chama hicho waliopigwa na polisi, kisha kulazimishwa kukiri kuwa walitumwa na viongozi wa Chadema kutekeleza matukio ya uhalifu.
Alisema kutokana na kitendo hicho, polisi inatakiwa kuchunguza na kutoa majibu sahihi huku akisisitiza kuwa hakuna mwanachama wa Chadema mkoani Dar es Salaam anayeweza kufanya tukio la aina hiyo.
Kilewo alitolea mfano matukio ya aina hiyo aliyodai kuwa yalifanywa na jeshi la polisi, yaliyowakuta aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Madaktari, Dk Stephen Ulimboka, kifo cha mwandishi wa habari Channel Ten, Daudi Mwangosi na sakata la Mhariri Mtendaji wa Kampuni ya New Habari (2006), Absalom Kibanda.
Yona ambaye ni Mjumbe wa Baraza Kuu la Chadema kwa sasa amelazwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), alikamatwa juzi na kisha kupigwa na baadaye kutupwa eneo la Tegeta Ununio na watu aliodai kuwa ni wafuasi wa Chadema.
Alisema watu hao walimtaka aache kuishambulia Kamati Kuu ya chama hicho iliyomvua madaraka aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho, Zitto Kabwe na kuwafukuza uanachama Dk Kitila Mkumbo (aliyekuwa Mjumbe Kamati Kuu) na Samson Mwigamba (aliyekuwa Mwenyekiti Chadema-Arusha).
Katika ufafanuzi wake Kilewo alisema: “Mwaka jana na mwaka juzi yalitokea matukio mengi ya aina hii. Kama mtakumbuka polisi waliwahi kumkamata mwanachama wa Chadema, Evodius Justinian na wenzake na kuwatesa, baadaye kuwashinikiza wakiri kuwa viongozi wa Chadema ndiyo waliwatuma kutekeleza matukio ya uhalifu.”
Aliongeza: “Kanda ya Dar es Salaam tunakijua chama vizuri, kimekuwa mstari wa mbele kutetea haki za binadamu, kupinga ukatili na uhuni hivyo hakiwezi kumtuma mtu yeyote kufanya vitendo kama hivyo vya utekaji, utesaji ama udhalilishaji wa aina yoyote.”
Chadema kipo tayari kuwachukulia hatua kali wanachama wake wasaliti na wanafiki na kwamba hakiwezi kumvumilia mtu yoyote anayehusiana na chama hicho endapo kitabaini kuwa amehusika katika tukio la kupigwa kwa Yona.
Alisema kuwa Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova anatakiwa kuacha kulitumia jeshi hilo kama kitengo cha propaganda za kisiasa, baada ya kamanda huyo kueleza kuwa Yona alidai kuwa amepigwa na wafuasi wa Chadema.
Katika maelezo yake ya juzi, Kamanda Kova alisema kufuatia tukio hilo ameunda jopo la wapelelezi wanane watakaoongozwa na Mkuu wa Upelelezi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP), Jaffari Mohamed kuchunguza tukio hilo.
VIA MWANANCHI.
Next Post Previous Post
Bukobawadau