Bukobawadau

NI KWELI NYERERE KAFA KWA HUZUNI

Na Prudence Karugendo
WIKI mbili zilizopita niliandika makala iliyobeba kichwa cha habari cha “Mandela katuachia fundisho, tutalitekeleza?” Katika makala hiyo nilijaribu kuyaangalia maisha ya Mandela, hasa baada ya kuanza harakati zake za kuutokomeza ukaburu,  akiwa uraiani, jela na baadaye uraiani tena, na kupata mtazamo kwamba maisha hayo ya Mandela yalikuwa ni fundisho kwa wanadamu wote wapendao haki, hususan Waafrika wenzake.
Lengo la makala hiyo lilikuwa kwamba haitoshi kumpongeza Madiba kwa hotuba nzuri tu kwa kuyatazama aliyoyafanya katika uhai wake na kisha kuyapiga kisogo. Kwa maana halisi ya kuyapongeza aliyoyaishi ni vena nasi tukajaribu kuyaishi yale yote aliyoyaamini.
Lakini ninachojiuliza mpaka leo ni kwamba tutaiweza hiyo changamoto aliyotuachia Madiba? Tutaweza kuishi kama alivyoishi yeye akiwa ameuweka umimi pembeni na kuitanguliza haki ya kila mmoja ambayo yeye aliiona ni bora  kuliko hata uhai wake? Kumbuka mara kwa mara alikuwa akitamka kwamba yeye anapigania haki ya wote, bila kujali rangi, kabila wala jinsia, muda wote akisisitiza kwamba ikibidi ni bora afe kwa hilo.
Mandela aliyoyapigania yote kayashuhudia yakitimia akiwa bado hai. Ukaburu ukatokomea, mfungwa maarufu duniani akatoka jela na kuwa rais wa kwanza mweusi nchini kwake, akakaa kipindi kimoja madarakani na kuwaachia wengine watawale. Umimi akiwa ameupiga kumbo.
Kwa upande wake, kweli Mandela kayatimiza yote aliyoyapigania, ndiyo maana nasema kwamba sidhani kama kuna mtu aliyepata kufa kwa furaha kama alivyokufa mzee wetu huyo. Sababu mambo yote aliyokuwa akisema kwamba yuko tayari kuutoa uhai wake ili yaweze kutimia yametimia bila uhaI wake kutoka! Ushindi ulioje?
Makala hiyo ilipotoka msomaji mmoja akanitumia ujumbe mfupi wa maandishi akiniuliza kwamba iwapo nasema kwamba Mandela kafa kwa furaha kwani Nyerere alikufa kwa huzuni?
Pamoja na kwamba halikuwa lengo langu kuilinganisha hiyo misiba miwili, hatahivyo nadhani hilo ni  jambo lisilohitaji mjadala kwa wale wenye uwezo wa kuchanganua mambo.
Kwa ufupi ni kwamba ingetokea yale yote aliyoyapigania Mandela yakaanza kubadilika akiwa hai, watu wakaanza kubaguana tena kwa misingi ya rangi na ukabila, haki za wadogo zikaanza tena kumezwa na mapapa nakadhalika, bilashaka  tungekuwa tunaongea mambo mengine juu ya Mandela kwa wakati huu. Hata mimi nisingeweza kusema Mandela kafa kwa furaha.
Tukiviangalia hivi vifo viwili, kifo cha Nyerere na kifo cha Mandela, tutayaona mambo mawili yasiyofanana hata kidogo. Kifo cha Nyerere ulikuwa ni musiba mzito, majonzi kila mahala hasa hapa nchini mwetu. Lakini kifo cha Mandela lilikuwa ni tamasha, watu wakiimba na kucheza kwa furaha, furaha ya kumuaga shujaa.
Mantiki ni kwamba mtu aliyefanikisha malengo yake ni shujaa. Mfano katika kabila la Wahaya akifa babu au bibi, mzee aliye na wajukuu, haisemwi kwamba kafa ila wanasema “yataya”. Sina tafsiri sahihi ya neno hilo kwa Kiswahili ila lina maana ya kutimiza ada ya maumbile, kwamba kizaliwacho ni lazima kife.
Kwahiyo kinachofuatia kwa Wahaya baada ya babu au bibi kufariki ni sherehe inayoendeshwa na wajukuu wa marehemu, wao wanaita “okusiribya”. Maana ya “kusiribya” ni kutania, sababu mjukuu ni mtani wa bibi au babu.
Kwahiyo wajukuu wanachukulia kwamba babu au bibi kayatimiza yote aliyotumwa na Mwenyezi Mungu. Kaoa au kuolewa, kazaa watoto nao wamezaa wengine, kipi tena ambacho bibi au babu angekifanya zaidi? Hivyo inachukuliwa kwamba kumlilia mtu wa aina hiyo ni sawa na kumkufuru Mungu.
Hivyo wajukuu wanafanya sherehe ya kumshukuru Mungu ikiwa ni pamoja na kuwaliwaza wazazi wao ili wasihuzunike sana kwa musiba wa mzazi wao ambaye kayatimiza yote yaliyomleta duniani.
Hiyo ni tofauti na anapokufa kijana. Kijana analiliwa na kila mtu, pengine kutokana na ukweli wa kwamba anakuwa bado anayo mengi aliyotakiwa kuyatekeleza. Kwahiyo kwa kijana Wahaya wanatumia usemi wa kwamba “omwana yagutuka” wenye maana ya kijana kakatika, sawa na kusema kijana kakatisha maisha yake.
Lengo la makala hii ni kujibu swali la msomaji aliyeniuliza kuwa kama nasema kwamba Mandela kafa kwa furahaa ina maana Nyerere kafa kwa huzuni?
Kitendo cha Nyerere kuliliwa na kila mtu kilikuwa na maana kubwa, hata kama waliolia si wote waliokuwa na uwezo wa kutambua kwa nini walilia. Maana yake ni kwamba waliolia walikuwa bado wanamhitaji Mwalimu, bila ya wote kuelewa kinagaubaga maana ya majonzi yao, ukweli unabaki palepale kwamba kazi ya Mwalimu ilikuwa bado haijatimia, au ilitimia baadaye ikapindishwa au kurudishwa nyuma!
Kwa mantiki hiyo, ndiyo maana nasisitiza katika makala hii kwamba Nyerere alikufa kwa huzuni tofauti na rafiki yake, Mandela, aliyekufa kwa furaha kubwa. Kwa nini nakuwa na mtazamo huo?
Tangu kabla Nyerere hajafa alianza kuonyesha namna alivyosikitishwa na mabadiliko yaliyokuwa yakijitokeza yakiyaondoa karibu mambo yote aliyoyatengeneza yeye na mambo hayo kuipa nchi yetu heshima ya pekee duniani kote.
Mwanzoni Nyerere alilalamikia kitendo cha wafanyabiashara, wengi wao wakiwa ni vijana, kuizoea Ikulu kiasi cha baadhi yao kufikia kumuita mke wa rais shemeji ilhali akiwa ni Mama wa Taifa! Katika hilo heshima ilikuwa imeporomoka wala siyo kupungua!
Baadaye Nyerere akalalamikia kitendo cha wabunge kujitenga na wapiga kura wao na kutaka wao waitwe waheshimiwa badala ya kuwa ndugu. Neno ndugu lilitutambulisha duniani kote, heshima ya pekee, lakini wabunge wetu wakalikataa wakidai kwamba wanapochaguliwa wanakuwa viumbe tofauti, siyo ndugu tena!
Baadaye Azimio la Arusha likapigwa teke! Nyerere akalalamika sana na kusema kwamba yeye hakuona kosa lolote la Azimio la Arusha, akaongeza kuwa lile lilikuwa ni azimio la utu. Akasema mfukoni mwake alikuwa anatembea na vitabu viwili, Biblia, kitabu cha Mungu,  na kile cha Azimio la Arusha.
Vilevile Nyerere akawa anashangaa na kasi ya wananchi kuanza kutambuana kwa makabila yao. Akatoa mfano jinsi alivyokwenda New York na kukaribishwa chakula na Mama Mongella, kule kwenye chakula akakutana na mama mmoja wa Kiganda aliyemweleza kuwa katika nchi nyingi za Kiafrika watu hutambuana kwa makabila yao lakini si katika Tanzania. Nyerere akamwambia mama huyo “mama hayo ni ya zamani siku hizi Watanzania wanatambuana mpaka kwenye vijiji wanakotoka!”.
Baada ya hapo ukaja ubinafsishaji wa mali za umma hasa zile zilizotaifishwa kufuatia Azimio la Arusha. Nyerere akasema kwamba mtabinafsisha mpaka Magereza!
Ndipo baadaye likaja suala la Muungano, Nyerere akasema iwapo Watanzania mtaingiwa na dhambi ya ubaguzi ya kusema wao Wazanzibari sisi Watanganyika, au sisi Wazanzibari wao Watanganyika, dhambi hiyo itawatafuna. Mpaka Mwalimu akatoa laana kwamba dhambi hiyo inabidi iwatafune ikiwa mtaiendekeza!
Na yawezekana laana hiyo ya Mwalimu imeanza kufanya kazi, sababu majuzi mjini Kigoma tulishuhudia kitu ambacho hatukukizoea. Watu walitayarishwa na kufanya maandamano wakiwa na mabango yenye maneno “Wachagga waende zao watuachie Kigoma yetu”! Ni lazima mambo hayo yanaandaliwa na kulindwa na watu waliofilisika kisiasa wakitafuta pa kujishikiza ili kupata uhalali wa kisiasa.
Zipo sababu mbalimbali zilizochangia kuihuzunisha roho ya Baba wa Taifa. Mbali na zile zilizokuwa katika uwezo wake wa kuzikemea, ipo moja kubwa iliyokuwa nje ya uwezo wake, nayo ni ya kufilisika kisiasa. Mwalimu aliwahi kusema kwamba mtu akifilisika kisiasa ni lazima atafute mahali pa kujishikiza kujenga uhalali wa kuendelea kuitwa mwanasiasa. Akasema mtu wa aina hiyo atatafuta ukabila, ukanda au udini. Hayo ndiyo tuliyoyashuhudia Kigoma!
Kisha akasema kwamba enzi zile za maadili mtu aliyeutamani uongozi wa umma alikuwa anaangaliwa ana mali kiasi gani, maana alisema kuwa mali ilikuwa “disqualification” ya kuupata uongozi, akasema kwamba kwa sasa mali diyo “qualification!” ya kwanza katika kuutafuta uongozi!
Vilevile Mwalimu alikuwa akisisitiza kwamba Ikulu ni sehemu takatifu, akisema kwamba pale hapauzwi nyanya, kwa maana ya kutofanywa biashara yoyote katika eneo lile. Lakini ajabu mtu ambaye Mwalimu alimpigania kumwingiza Ikulu akiwa na imani kwamba angeweza kuyalinda maadili hayo, bila aibu wala haya, mtu huyo akaja kusajili kampuni ya biashara akijitambulisha kama mjasiriamali anayeishi Ikulu!
Hayo na mengine ndiyo yanayonifanya niamini kwamba Nyerere alikufa kwa huzuni mkubwa, kwa hayo hawezi kufanana na Mandela hata kidogo.
0784 989 512
Next Post Previous Post
Bukobawadau