Bukobawadau

BUNGE LA KATIBA LAZUIA WAANDISHI WA HABARI

Bunge Maalumu la Katiba limepitisha kanuni ya kuwazuia waandishi wa habari kuingia katika vikao vya kamati za chombo hicho, hatua ambayo inaelezwa ni kinyume na Katiba inayotoa uhuru wa wananchi kupata habari.
Kanuni hiyo ilipitishwa jana baada ya malumbano makali yaliyowagawa wajumbe wa bunge hilo, baadhi wakipinga kifungu hicho kwa sababu kinavunja Katiba ya nchi inayotoa uhuru kwa waandishi kukusanya na kusambaza habari na wengine wakiunga mkono kuwazuia.
Kanuni hiyo ilipitishwa kwa mbinde huku baadhi ya wajumbe wakiendelea kushikilia msimamo wa kuikataa, hata baada ya Mwenyekiti wa Muda wa bunge hilo, Pandu Ameir Kificho kuridhia kipite. Wajumbe waliopinga kanuni hiyo ni Joshua Nasari, Moses Machali, Peter Serukamba, Ezekiah Wenje na Maria Sarungi.
Baadhi ya wajumbe akiwamo Katibu Mtendaji wa Baraza la Habari Tanzania (MCT), Kajubi Mukajanga walisimama kutaka kuzungumza lakini hawakupata fursa hiyo.
Mjumbe aliyekuwa mwiba kwa Tasnia ya Habari ni, Dk Harrison Mwakyembe ambaye aliwashawishi wajumbe kufunga mjadala huo ili wasonge mbele kwa madai kuwa hata yeye pia ni mwanahabari. "Hakuna upande usiotambua umuhimu wa vyombo vya habari katika mchakato huu... Tunachotofautiana ni jinsi na namna
ya ushiriki wa vyombo vya habari," alisema Dk Mwakyembe. Alisema Taifa limeingia katika kipindi maalumu kama cha vita na kwa msingi huo, kanuni zinabadilika kulingana na mazingira na kwamba vyombo vya habari vinapaswa kulitambua hilo.
Hata hivyo, Kifungu cha 57 (3) katika kanuni hiyo kilipita baada ya kufanyiwa marekebisho kuondoa maneno 'mwenyekiti anaweza kutoa taarifa' badala yake, ikawa 'ni lazima kutoa taarifa.'
Kanuni hiyo inampa mamlaka mwenyekiti wa kamati au mjumbe yeyote kwa idhini yake, kutoa taarifa kwa vyombo vya habari kuhusu mambo yaliyojitokeza kwenye kikao.
Mjadala wakwama
Mvutano juu ya kifungu hicho ulianza juzi jioni wakati baadhi ya wajumbe walipotofautiana.
Akiwasilisha maoni ya Kamati ya Kumshauri Mwenyekiti, Mjumbe George Simbachawene alisema iwapo waandishi wataruhusiwa wangeweza kutoa taarifa zisizochujwa ambazo zitawachanganya wananchi.
Hata hivyo, Mjumbe wa bunge hilo, Ezekiah Oluoch alisema kisheria kanuni hiyo ilikuwa inakwenda kinyume na Ibara ya 18 ya Katiba ya nchi ambayo kimsingi, ndiyo sheria mama. Aliisoma ibara hiyo akisema kama wajumbe wataruhusu kupitishwa kwa kifungu hicho, litakuwa kosa kubwa la kuvunja katiba ya nchi.
Ibara hiyo ya 18 ya katiba inasomeka, "Kila mtu anayo haki ya kutafuta, kupokea na kutoa habari bila kujali mipaka ya nchi... anayo haki ya kupewa taarifa wakati wowote kuhusu matukio muhimu kwa maisha na shughuli za wananchi, pia kuhusu masuala muhimu kwa jamii."
"Hapa tuko kwa masuala muhimu kwa jamii kama waandishi wa habari wa Tanzania wana matatizo katika kuripoti habari za Bunge, hilo ni tatizo jingine, hatuwezi kutunga kanuni zinazokwenda kinyume na Katiba ambayo ndiyo sheria mama," alisema.
Akichangia hoja hiyo, Mjumbe Halima Mdee alisema: "Namshangaa Mheshimiwa Simbachawane kwani yeye ni Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano na anajua kwamba waandishi wanaruhusiwa kwenye vikao vya kamati. Iweje hapa kwenye Bunge la kutunga Katiba?
"Ninachokiona ni kwamba waandishi wa habari wanakatazwa kwa sababu ya hofu. Hii siyo Katiba ya kikundi cha watu 629 tuliopo hapa. Hii ni Katiba ya wananchi na wanayo haki ya kujua majadiliano yanayoendelea katika Kamati."
Mjumbe Machali alisisitiza kuwa kuwazuia waandishi ni kukiuka Katiba na kuhoji: "Nyie mnaosema mnataka kura za wazi ili wananchi wajue, mnaogopa nini? Katika hoja hiyo, Mjumbe Freeman Mbowe alisema Katiba ni mali ya wananchi na kwamba wana haki ya kufahamu kila kinachoendelea ndani ya Bunge.
"Kuna Watanzania kwa mamilioni ambao wanatusikiliza, kinachoonekana hapa tunaanza kuweka mkakati wa kuchuja nini kipelekwe kwa wananchi na hii ni hatari sana katika mchakato wa Katiba," alisema.
Alisema vyombo vya habari vina umuhimu wa kuripoti kila kinachoendelea ndani ya kamati na utaratibu wa kuwaruhusu waandishi wa habari kuripoti katika kamati umetumika katika nchi za Kenya na Afrika Kusini.
Baada ya hoja hizo za juzi usiku, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Profesa Costa Mahalu alisema: "Wajumbe ndiyo mnaokubali au kukataa mapendekezo yaliyotolewa na kamati yetu. Sisi mnatuagiza tunarekebisha mwafaka uliofikiwa na wajumbe na kuonyesha msimamo wao kwa pamoja, naomba hili tulirudishe kwa wajumbe wenyewe waliamue."
Hata hivyo, malumbano zaidi yaliendelea jana na Mwenyekiti Kificho alitoa taarifa ya kukubaliana na mapendekezo ya kamati yake.(P.T)
Chanzo:Mwananchi
Next Post Previous Post
Bukobawadau