Bukobawadau

CHAMA KIPYA CHA ACT CHASHUSHA BENDERA ZA CHADEMA KIGOMA

CHAMA cha Alliance For Change and Transparency Mkoa wa Kigoma,kimeshusha Bendera ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA tawi la Ujiji stendi ya zamani na kupandisha bendera ya (ACT) wakati wa uzinduzi rasmi wa matawi sita katika manispaa ya kigoma ujiji.

Akizungumza na wananchi wa eneo hilo, Katibu wa ACT Mkoa Athuman Kabogo alidai lengo la kushusha bendera hiyo ni hatua ya kukataa kugeuzwa kuwa vibaraka wa watu wengine kwa kukosa haki ya kuhoji na kuwania nyadhifa za chama hicho na
hivyo kuanzisha ACT kama chama cha wanyonge kinachoweza kuwasikiliza na kutoa haki kwa kila mmoja.

Kabogo aliwataka wanachama wahitaji, wachukue kadi za ACT ili chama kipate usajili kamili kwa mujibu wa sheria,kanuni na taratibu husika pamoja na kutoa michango endelevu ,ikiwa ni jitihada za makusudi kuhakikisha chama kinasonga mbele
kwa maslahi ya Taifa.

�Wananchi nyie ni chachu ya chama kuwepo kwenye mchakato wa uchaguzi mdogo wa wenyeviti wa serikali za mitaa kwa kukiamini na kukipatia ridhaa kiweze kuleta
mabadiliko ya kimaendeleo� alisema Juma Ramadhan aliyekuwa katibu kampeni wa CUF kigoma.

Kwa upande wa Katibu ACT Kanda Magharibi Wiston Moga alisema, lengo la chama ni kuleta mabadiliko kwenye ulingo wa siasa,ambapo wao wamedhamiria kutetea maslahi ya umma kwa lengo la kuondoa mfumo wa maslahi binafsi ambayo ni chachu ya vyama vya siasa kushindwa kuleta mabadiliko chanya kwa wananchi.

Katika ziara hiyo ya uzinduzi wa matawi ya chama husika,ACT kimefanikiwa kufungua matawi kwenye kata sita kati ya kata 19 zilizopo katika manispaa ya kigoma ujiji,huku baadhi ya viongozi kutoka UPD,CHADEMA na CUF wakijiunga na chama hicho
kwa kudai wanahitaji chama chenye uchungu na kukabiliana na changamoto za wanyonge.

Hata hivyo wanachama 3500 wa chama cha Democrasia na Maendeleo Chadema katika tawi la Ujiji mkoani Kigoma wamehamia chama kipya cha Alliance For Change and Transparency (ACT).
Next Post Previous Post
Bukobawadau