Bukobawadau

MCHAKATO WA KATIBA MPYA:Ya Kaizari yanapochanganywa na ya Mungu!

Na Bernard Kazinduki
MCHAKATO  wa Katiba Mpya unaonekana kuingiliwa kwa nguvu na wasiopaswa kuuingilia. Tena wanauingilia kwa mtindo wa kuhatarisha mustakabali wa nchi yetu. Maaskofu 32  wa Kikristo wameuingilia  mchakato huo kwa kutumia mamlaka walio nayo ya uongozi wa kiroho na kutaka  kuwafanya wananchi waamue kulingana na maelekezo yao hao viongozi wa kiroho.
Maaskofu hao wanafanya hivyo wakiwa wameyasahau maelekezo muhimu ya aliye muhimili wa imani yao, aliyewafanya wakaabudu kwa jina lake, yaani kujiita Wakristo, Yesu Kristo mwenyewe.
Katika kuepusha mgongano wa mamlaka, mgongano wa mamlaka ya kidunia na ya Kimungu, Kristo alishauri kwamba ya Kaizari mpeni Kaizari na ya Mungu mpeni Mungu. Kwa kauli hiyo tayari Kristo alikuwa ametenganisha mambo ya Mungu, kiimani, na masuala ya mamlaka ya kidunia. Alitenganisha dini na siasa.
Kristo hakutaka watu wavunje sheria za kidunia kwa kisingizio cha imani ya kumtii Mungu. Sababu hata Mungu anataka mamlaka halali ya kidunia yaheshimiwe, walio na utiifu kwa mamlaka ya kidunia ndio walio katika mwelekeo wa kumtii yeye Mungu.
Ipo mifano mingi inavyoonyesha kwamba Mungu anawataka waja wake wayatii mamlaka ya kidunia. Mfano mmojawapo ni wa mfalme wa Uganda, Kabaka Mwanga wa Pili. Kabaka huyo  aliwakataza watu wake kufuata mafundisho ya imani za kigeni, lakini baadhi ya watu walikaidi wakaendelea kufuata mafundisho hayo ya imani za kigeni.
Alipowakamata wasaliti hao wa amri yake, hasa wale 22 waliokuwa  wahudumu wa Ikulu, akawachoma moto na wengine kuwakaanga kwa mafuta ya kula kama “kiti moto” huku akisema kwamba kama Mungu yupo wanayefundishwa na wazungu basi na aje auzime moto huo.
Mungu hakuuzima moto huo, watu hao waliungua na kufa. Mimi naamini kwamba Mungu hakushindwa kuuzima moto huo ila alitaka ya Kaizari apewe Kaizari na ya kwake apewe yeye. Ni wazi kwamba Mungu hakufurahishwa na ukaidi wa watu hao kwa kiongozi wao wa kimwili.
Nchi yetu ya Tanzania muda wote imekuwa na amani tangu ilipopata Uhuru wake ikiwa Tanganyika na baada ya kuungana na Zanzibar kuwa Tanzania. Kilichoifanya amani ikatamalaki muda wote, zaidi ya miaka 50 sasa, pamoja na mambo mengine, ni hekima ya viongozi wake ya kutochanganya mambo ya Mungu na ya kidunia. Kwahiyo sidhani kama Kristo alikosea kutowataka watu kuchukua yaliyo ya Kaizari na kumpa Mungu. Alijua kwamba kwa kufanya hivyo ni lazima kungetokea mtafaruku katika jamii.
Katika mchakato huu wa kutafuta Katiba Mpya ya nchi yetu, yawezekana kweli maoni ya wananchi walio wengi kuhusu muundo wa Muungano wetu yakawa ni kuwa na serikali tatu. Lakini hiyo haitoshi kuufanya muundo wa muungano wetu uwe wa serikali tatu, ni lazima iangaliwe pia hali hiyo ya wananchi kutamani kitu ambacho kinaonekana si salama kwao inatokana na nini. Inawezekana watu walio wengi wakawa wamepatwa na dhambi ya ubaguzi.
Dhambi ya kwamba “wao Wazanzibari sisi Watanganyika”. Dhambi hiyo ni ya hatari kabisa, na kama alivyosema Baba wa Taifa, dhambi hiyo inatafuna pale inapokumbatiwa. Kwa nini maaskofu wetu hao wanashindwa kuliona hilo?
Kusema kwamba maoni ya walio wengi yaheshimiwe bila kutumia hekima ya kuangalia ni maoni ya aina gani ni uzembe mkubwa kiuongozi. Ikumbukwe jinsi Watanzania asilimia 82 walivyotaka mfumo wa  chama kimoja cha siasa uendelee hapa nchini lakini hekima za Baba wa Taifa zikaonyesha kwamba pamoja na mambo kuwa hivyo mfumo vyama vingi hakuwa na sababu yoyote ya kuzuilika. Hivyo asilimia 18 ikaishinda asilimia 82!
Muundo wa serikali tatu katika Muungano wetu utajenga ubaguzi wa kuwaona Wazanzibari kama sio wenzetu. Ni tofauti na ilivyo kwa sasa, tunawaona Wazanzibari  kama wenzetu wakati wao wanaendelea kuwa na serikali yao ya Zanzibar. Hiyo ni kwa sababu kwa idadi yao ilivyo hakuna uwezekano wowote wa kwamba wanaweza kuimeza  idadi kubwa ya Watanganyika.
Lakini tukisema tuwe na serikali moja, kwa maana ya kuwa na Tanzania tu bila serikali ya Zanzibar, uwezekano wa Wanzibari kumezwa katika muungano wa aina hiyo ni mkubwa sana, sababu idadi yao ni ndogo. Hicho ni kitu ambacho  hakuna anayekitamani, awe Mzanzibari au Mtanganyika. Sasa kama asilimia 18 iliishinda asilimia 82 katika mfumo wa vyama vya siasa,  kwa nini asilimia zaidi ya 40 ionekane imekufuru kwa kuishinda asilimia iliyo chini ya 60 katika muundo wa muungano?
Lakini kuiacha Zanzibar iwe na serikali yake huku Tanganyika nayo ikiwa na serikali yake katika muundo wa serikali tatu uwezekano wa kutafunwa na dhambi ya ubaguzi, wao Wazanzibari sisi Watanganyika, ni mkubwa sana. Na tusije tukasahau kwamba Baba wa Taifa alishautolea radhi ubaguzi wa aina hiyo.
Viongozi hao wa kidini kwa nini hawataki kujifunza kutoka kwa viongozi wenzao wa kidini katika nchi ya Rwanda? Katika nchi hiyo ya Rwanda viongozi wa kidini, mapadri na maaskofu, waliichochea dhambi ya ubaguzi wakionyesha kwamba wao Watutsi na sisi Wahutu, matokeo yake ni mauaji ya kimbari yaliyoitetemesha dunia nzima.
Ni kwa mantiki hiyo nashindwa kuyatilia maanani maoni ya maaskofu hao 32 ya kwamba maoni ya wananchi ya serikali tatu yaheshimiwe.  Sababu viongozi wenye hekima hawapaswi kufuata tu idadi bali hekima vilevile. Sidhani kama wakija ibilisi watatu askofu atalazimika kukubaliana nao kwa kuheshimu wingi wao na kumuacha malaika mmoja kwa vile yuko peke yake.
Kwa maana hiyo tunapaswa kuangalia mantiki ya kitu imekaaje bila kujali wingi wa watu wanaokitaka. Tusikurupuke kukitamani kitu kinachoonyesha kitatupeleka kwenye maangamizi kwa kuangalia tu wingi wa wanaokitamani.
Kwahiyo katika hili ni vema tukaeleweshana uzuri na ubaya wa tunachokiongelea bila kugombana wala kutukanana. Viongozi wetu wa kiroho inabidi nao tuwasahihishe kiungwana pale tunapoona wamejisahau na kukifanya kitu kilicho kinyume na mafundisho ya kiroho wanayopaswa kuyafuata.
Kristo aliposema kwamba ya Kaizari apewe Kaizari na ya Mungu apewe Mungu, alikuwa na maana kubwa. Kikubwa alichokilenga ni kutogonganisha mambo ya kiroho na yale  ya kimwili. Kwahiyo maaskofu wetu hao wanapaswa kuuzingatia ushauri huo wa Kristo.
MUNGU IBARIKI TANZANIA
Next Post Previous Post
Bukobawadau