Bukobawadau

TUACHANE NA UPUUZI WA PICHA ZA MITANDAONI

Na Prudence Karugendo
NIMESHANGAZWA  na kusikitishwa sana na habari iliyotanda kwa sasa nchini kuhusu picha za kipuuzi zinazotolewa kwenye mitandao ya kijamii. Picha hizo zimefikia hata kuliteka Bunge letu, wabunge wameharibu muda wa kujadili mambo nyeti yanayowagusa wananchi na nchi kwa ujumla na badala yake wakajikita katika kuzijadili picha hizo za kipuuzi!
Picha hizo, ziwe za kweli au za kutengenezwa kwa njia ya teknolojia ya kisasa, bado ni za kipuuzi kiasi kwamba kuacha mambo muhimu na kuzijadili au kuhangaika nazo kwa namna yoyote ile ni utovu wa uadilifu.
Sababu kuna mfano unaotolewa kwamba ukiwa unaoga mtoni akapita kichaa akakwapua nguo zako na kukimbia nazo, wewe kwa hasira ukaamua kumkimbiza ukiwa uchi, nani ataonekana ni kichaa? Bilashaka wewe uliye uchi ndiye utaonekana kichaa!
Mimi naamini kwamba tunachokihitaji kwa sasa ni maendeleo yenye kuleta maisha bora tukiwa tumeziangalia nchi zilizotutangulia kimaendeleo na kuyafikia hayo maisha bora. Tuangalie zinafanya nini na kupuuza nini ili tuige.
Wingereza kwa mfano, wakati fulani Malkia Elizabeth II, alikuwa anateremka kwenye ndege upepo ukainua nguo yake na kuonyesha sehemu yake ya ndani, wanahabari waliokuwa pale wakapiga picha na kuitoa kwenye magazeti kwa kichwa cha habari “A royal thigh” kwa maana ya paja la kifalme! Picha hiyo haikujadiliwa mahala popote na mamlaka yoyote ya Kingereza.
Wakati mwingine, kulekule Wingereza, mtoto wa kifalme, Prince William, akiwa mdogo akicheza kwenye busitani akaamua kukojoa kulekule kwenye busitani, mapaparazi wakamuona na kumpiga picha. Baadaye picha hiyo ikawekwa gazetini na kupewa kichwa cha habari “A royal wee”, tafsiri isiyo rasmi, mkojo wa kifalme!
Wangereza hawakushughulika na picha hizo sababu hazikuingiliana  kwa namna yoyote na mambo yao ya kimaendeleo. Waliacha upuuzi ubaki upuuzi.
Hata Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, aliwahi kusema kwamba kuna wakati “aliwakoromea”  Wangereza nyumbani kwao kuhusu Rhodesia, Zimbabwe kwa sasa, kesho yake magazeti ya kule yakatoa picha yake akiwa na mkia kama panya. Nyerere hakujali,  maana aliona ni upuuzi ambao haukuweza kuzuia nguvu ya ukweli aliokuwa akiutoa kuhusu unyama wa nchi hiyo kule Zimbabwe.
Mfano mwingine ni wa Marekani,  zilitoka picha nyingi za rais wa nchi hiyo, Clinton, akionekana amewambwa kwenye kinena cha mwanamke aliye uchi, Monica Lewinsky, lakini taifa hilo lililopiga hatua kimaendeleo,  halikuujali upuuzi huo kwa vile haukuzuia lolote katika maendeleo yake.
Tunachopaswa kuelewa ni kwamba tunapowachagua wabunge wetu tunaupima tu uwezo wao wa kutuwakilisha na kutusemea tunayoyahitaji, wala hatuangalii kama mtu kaoa, kaolewa, ana wapenzi wangapi nakadhalika. Maana hayo ni mambo yake binafsi, kuyafuatilia hayo ni kukosa mwelekeo. Ni sawa na kumfukuza ukiwa uchi kichaa aliyekwapua nguo zako wakati ukioga mtoni.
Kwahiyo picha ya Komba akiwa na “vimwana” inatugusaje iwapo yeye anatimiza yote aliyotumwa na wananchi wa Mbinga anaowawakilisha? Sababu mbali na kuyasema mahitaji ya wapiga kura wake Bungeni,  hawajamueleza afanye nini nje ya uwakilishi wake, ale nini, anywe nini, aongee na nani, nakadhalika. Hayo ni mambo yake binafsi.
Mimi binafsi, ugomvi wangu kwa Komba ni kauli yake aliyoitoa Bungeni ya kwamba ataenda msituni ili atuue na kuiharibu nchi yetu kwa kuyatetea na kuyalinda maslahi yake binafsi. Lakini siyo picha hizi za kipuuzi.
Ajabu kauli ya Komba kwenda msituni haikupigiwa kelele kama ilivyo kwa picha zinazoonyesha sura yake kwenye mtandao! Picha hizi za Komba akiwa na wanawake, hata kama ni za kweli, zina kitu gani cha kutudhuru kama ambavyo anaweza kutudhuru akiwa msituni anakotamani kwenda iwapo maslahi yake hayatazingatiwa?
Mimi nahisi kwamba pengine hiyo ni changamoto kwa kiwango chetu cha kutafakari. Maana tunapoacha kuyashughulikia mambo yanayotishia uhai wetu na badala yake kuyapigia kelele mambo yasiyo na maana wala athari yoyote, ni lazima ionekane kuwa kuna upungufu mkubwa katika fikra zetu.
Kuhusu maadili, vilevile lipo la kutazamwa. Wabunge wetu kuonekana katika picha za ufusika,  na nchi yetu kujigeuza “Matonya” ombaomba maarufu, kiasi cha kuomba hata pesa ya kuendesha mambo yake ya ndani, Bajeti, wakati nchi ikiwa imejaa utajiri wa asili usiosemeka, ni kipi kinachokosa maadili zaidi kati ya hivyo viwili?
Tuseme Tanzania inazingatia maadili na Marekani haizingatii maadili, lakini mbona maadili yetu hayatuzuii kuwa ombaomba kwa Marekani isiyozingatia maadili? Kwa nini hatuoni kuwa suala la maadili tunaloliimba kila wakati ni la kujidanganya tu?
Inafaa kwanza tuuone ukosefu wa maadili wa nchi kujigeuza ombaomba wakati imeulalia mlima wa utajiri kabla ya kuuangalia ukosefu kiduchu wa unadilifu wa wabunge wetu.
Tukumbuke kwamba wabunge sio malaika, ni binadamu kama tulivyo sisi wote. Wanayo mahitaji ya kawaida na matamanio ya kimwili kama walivyo wananchi wote. Mbali na tunayowatuma Bungeni, vilevile nao wanahitaji kusitarehe na kuburudika.
Labda kama picha hizo zingewaonyesha wabunge wanafanya uporaji wa mali ya umma, kinyume na dhima ya uwakilishi wao, hapo ndipo ningekuwa naongea vingine. Lakini picha hizi zinazoonyesha mambo yao ya faragha yasiyotuhusu naona ni uzumbukuku kuzipigia kelele.
Historia ya karibuni ya nchi ya Marekani inawataja marais wawili wa nchi hiyo waliopendwa sana na Wamarekani kutokana na kufanya mambo kadri ya mapenzi ya wananchi yalivyokuwa, kuliongoza taifa hilo kwa mafanikio makubwa. Marais hao ni John F. Kennedy (JFK) na William Jefferson (Bill) Clinton.
Lakini historia hiyohiyo ikiwatazama watu hao katika mambo yao ya faragha inaonyesha jinsi walivyokuwa wachafu kupitiliza. Ila kwa vile uchafu huo ulihusu tu mambo yao binafsi, Wamarekani mpaka leo hawaujali uchafu huo. Wao wanakijali kile walichowatuma wakifanye, ambacho marais hao walikifanya kwa ukamilifu na uadilifu mkubwa.
Kwa maana hiyo, hata sisi Watanzania, kama tunaitakia nchi yetu historia safi yenye mwelekeo wa maendeleo, hatunabudi kuachana na fikira potofu za kuyaweka mbele mambo madogo madogo na mepesi kama haya ya picha za kwenye mitandao, tena yanayolenga kwenye ufaragha, hata kama watu wanaolengwa ni viongozi wetu. Sababu hayo ni mambo yao binafsi yasiyoingiliana hata kidogo na dhamana tuliyowapa.
Katika kuonyesha kuchanganywa na picha hizo, kuna mbunge aliyesema uwekwe utaratibu wa wabunge kupatiwa ulinzi! Sikubaliani kabisa na hoja hiyo kwa sababu mbili ninatakazozitaja hapa chini. Moja ni kwamba kila mwananchi atahitaji ulinzi binafsi, sababu thamani ya uhai wa mbunge ni sawa na ya mwananchi yeyote mwingine.
Pili ni kwamba kwa mahitaji hayo ya mbunge ni sawa na kukiri kuwa uchafu unaoonyeshwa kwenye picha hizo za faragha ni wa kweli, kwahiyo walipakodi inabidi waugharamie ili uendelee bila bughudha!
Kwahiyo inabidi tuwaulize kina Komba kama wanakubali kuwa picha hizo ni za kweli ili tusilipie hewa, na kama wanaona inafaa walipakodi waugharamie uchafu huo kwa kuwawekea ulinzi ili usiendelee kupigwa picha. Lakini kama wanazikataa yanini kuweka ulinzi?
Mwisho, niseme kwamba tuachane kabisa kuhangaika na mambo ya kipuuzi kwa kusingizia neno maadili. Tunapaswa tuyaangalie maadili yetu kwa kuuchukia sana ufisadi ambamo ndimo kumejaa uvunjifu mkubwa wa maadili unaokaribia kuiangamiza nchi yetu, sio picha hizi za kutengenezwa kwenye mitandao. Hizo haziwezi kuiathiri nchi yetu kwa namna yoyote ile.
0784 989 512
Next Post Previous Post
Bukobawadau