Bukobawadau

ULEVI NA UVUTAJI NDIYO MIHIMILI YA UCHUMI WETU?

 Na Prudence Karugendo

NIMEJIWA  na wazo kwamba neno la tahadhari kwenye sigara na matangazo ya bidhaa hiyo lisemalo “ uvutaji wa sigara ni hatari kwa afya yako” ni la kuondoa kabisa. Sababu kwa maana nyingine neno hilo ni sawa na kusema  ukuzaji wa uchumi wa nchi yetu ni hatari kwa afya zetu.
 Lingine ni kwamba sheria ndogondogo kama ya kutofungua baa wakati wa kazi na kulazimisha baa kufungwa ifikapo saa sita usiku inabidi nazo ziondolewe. Sheria hizo zinaonekana kuuhujumu uchumi wetu.

Hiyo ni pamoja na kuwakamata walevi kwa kisingizio cha kulewa wakati wa kazi au kutembeza ulevi hadharani.

Kwa kadri mambo yalivyo hapa kwetu, walevi na wavuta sigara ni watu muhimu sana katika uchumi wa nchi yetu. Sidhani kama kuna kazi yoyote nyingine inayochangia katika ukuzaji wa uchumi wa nchi yetu kama walivyo walevi na wavuta sigara. Nitaeleza.

Kwa kipindi cha zaidi ya miaka 30 iliyopita, kila mwaka Hazina ya nchi wakati wa Bajeti, ni lazima ikachungulie kwa walevi na wavutaji kuangalia kuna nini cha kukusanya,  kana kwamba hizo ndizo sehemu pekee za ukusanyaji wa mapato yake!

Ni nani sasa asiyeona kuwa kuwasumbua  watu hao, wateja wa sigara na pombe, kwa sheria na tahadhari nilizozionyesha hapo juu,  ni kuuvuruga uchumi wa nchi?

Kama nchi haiwezi kuviangalia vyanzo vingine vya mapato zaidi ya sigara na pombe, kwa nini isiwaheshimu na kuwaendekeza watumiaji wa vitu hivyo muhimu kwa uchumi wake? Maana kwa nchi iliyo makini ni lazima iviheshimu vyanzo vya uhai wake. Uchumi kwa nchi ndiyo uhai wake.

Mfano, nchi za Sudan na Misri zinayaheshimu maji ya mito ya Nile, Blue Nile na White Nile. Kutokana na nchi hizo kunufaika na maji hayo, ipo imani kwamba maji hayo ni neema yao kutoka kwa Mungu ili kuulinda uhai katika nchi hizo.

Watu wa nchi hizo wako tayari kufa na yeyote anayejaribu kuyachezea maji ya mito hiyo kiasi cha kuyafanya  yaache kutiririka kuelekea kwao. Huo ndio umakini katika kukilinda kinachoonekana kinaulinda uhai katika nchi husika.
Mfano mwingine ni wa nchi ya Mauritius. Uchumi wa nchi hiyo kwa kiasi kikubwa unategemea kilimo cha miwa iliyochukua asilimia 90 ya ardhi yote iliyolimwa katika nchi hiyo.

Kwa vile zao la miwa ni mhimili wa uchumi wa nchi hiyo, linaheshimiwa sana na watu wa nchi hiyo. Wao wanasema chezea kingine lakini sio kuchezea miwa. Sababu kuchezea miwa ni sawa na kuchezea uchumi wa nchi yao. Wananchi wote wa nchi hiyo wanalielewa vizuri hilo.

Sasa kama Tanzania inategemea zaidi sigara na pombe katika uchumi wake, kwa nini watumiaji wa vitu hivyo wasipewe heshima kama ilivyo kwa nchi nilizozitaja namna zinavyoyajali mambo yanayohusiana na uchumi wake?

Kama kweli upo umakini katika kuulinda na kuukuza uchumi wetu, kwa nini matangazo ya tahadhari kwa wavutaji na bughudha kwa walevi tusivichukulie kama uadui dhidi ya nchi yetu sawa na Sudan na Misri wanavyowachukulia wanaojaribu kuchezea maji ya Nile ili yasitiririke kuelekea kwao?

Tofauti na dhana nzima ilivyo, Tanzania ni nchi iliyojaaliwa mambo mengi ya kuiinua kiuchumi. Ni nchi tajiri sana kwa upande wa maliasili, sema utajiri huo hauguswi linapokuja suala la mpangilio wa uchumi wake. Badala yake wahusika wanaviangalia tu vitu vidogovidogo kama pombe na sigara!

Lakini vitu hivyo sio vya lazima katika maisha ya mwanadamu japo wachumi wetu wamevipa kipaumbele kama mhimili wa uchumi wa nchi. Je, iwapo Watanzania wataamua kuachana navyo, wakaacha kulewa na kuvuta sigara, hayo mapato ambayo Waziri wa Fedha anayaangalia kila mwaka kwa upande huo atayatoa wapi?

Kwa nini tuache kutazama mapato ya kwenye vyanzo vya uhakika, kama vile kwenye utajiri wetu wa asili tuliojaaliwa nao, na badala yake tuendelee na hivi viini macho? Utajiri wetu tunauacha unasombwa na wageni kwa kisingizio cha kuwavutia wawekezaji! Ni lini tutanufaika na hao tunaowavutia na kuacha kuwategemea wavutaji na walevi?

Wakati baadhi ya wawakilishi wa wananchi, wabunge, wakilalamikia Bajeti ya mwaka huu katika Bunge linaloendelea, mbunge mmoja aliyeondolewa kwenye uwaziri kwa tuhuma za ufisadi, amewakebehi wabunge wenzake hao akidai kwamba wanawapotosha wananchi. Yeye anadai wananchi wanaifurahia Bajeti ya mwaka huu.

Lakini baadhi ya wananchi wa Jiji la Mwanza wanasema kwamba mbunge huyo asitake kuigeuza furaha yake kuwa ni ya wananchi wote. Wanasema furaha aliyo nayo yeye inatokana na ukwasi alio nao ambao hawana hukakika kama anaweza akautolea maelezo namna alivyoupata.

Nikiwa Jijini humo,  nikaonyeshwa hoteli moja yenye ghorofa 9 iliyoko Mtaa wa Rufiji, nikaambiwa kuwa ni mali ya mbunge huyo anayeona raha ya maisha akiwachukulia Watanzania wote kuwa wana raha ya maisha kama aliyo nayo yeye. Lakini wanasema kwamba hoteli hiyo imeandikwa kwa jina la ndugu wa mbunge huyo ili kujaribu “kuwazuga” watakaotaka kuifuatilia.

Wananchi wengine wanaamini kwamba yanayosemwa na mbunge huyo ni upotoshaji katika kuficha dhana ya kwamba kuna wananchi wanaolalamikia ugumu wa maisha, kwa vile mbunge huyo anaelewa ni kiasi gani alivyouchangia ugumu huo kwa kujilimbikizia mali ikiwemo hoteli hiyo katika Mtaa wa Rufiji Jijini Mwanza.

Wananchi hao wanasema kwamba wao watafurahi, kama yeye anavyodai, iwapo ataweza kuutolea maelezo utajiri aliojilimbikizia kwa muda mfupi. Sababu wanasema wengi wanamuelewa tangia kijijini kwao mpaka hapo alipo, matawi ya juu!

Godfrey David Mollel ni mkazi wa mji wa Arusha, anasema “Niko njiani naelekea nyumbani,  nimekutana na mwanamke, anaonekana katoka kujifungua sababu kabeba kichanga chenye umri wa masaa tu. Inaonekana mama huyu kakosa nauli na kuamua kutembea kwa mguu na hali hiyo aliyo nayo!”

Mwananchi huyo wa Arusha anauliza, haya ndiyo maisha bora kwa kila Mtanzania tuliyoahidiwa? Anaongeza, “Mwanamke huyo aliyetoka kujifungua na kulazimika kutembea kwa mguu kwenda nyumbani kwake naye anaifurahia Bajeti ya mwaka huu kama anavyodai mbunge huyo mkwasi?”

Nikirudi kwenye mjadala wangu ningetaka kuuliza hivi, katika historia ya dunia ni wapi panapotajwa kuwa nchi zilizoendelea mwanzo wake ulikuwa ni kuwavutia wawekezaji toka kwingine wakaende  kupora utajiri wa nchi hizo na kuuhamishia kwao? Na kama hilo halimo kwenye historia ujasiri wa kwamba linaweza kutusaidia sisi tunautoa wapi?

Kinyume chake historia inatuonyesha kuwa kila kilichopatikana katika nchi zilizoendelea kilihakikishwa kinazinufaisha nchi husika, na ilipowezekana kingine kiliporwa kwingine na kuongezewa, ndiyo maendeleo tunayoyaona kule.

Lakini kwetu sisi ni tofauti, tunawavutia wawekezaji toka nje waje kusomba utajiri wetu kadiri wanavyoweza, na wakati mwingine tukisaidiana nao kuipora nchi yetu kwenda kuficha kwao!

Ndipo zinapokuja fikra za kutaka kuwa na uraia wa nchi zaidi ya moja kusudi “kikinuka” huku kwetu tugeuke raia wa Ughaibuni na kuwaachia manyoya wenye kutaka kuleta za kuleta!

Kwa fikra za aina hiyo, kutaka kuwa na uraia wa zaidi ya nchi moja, upo uwezekano wa uzalendo hapo unaoweza kumsukuma mtu ayafikirie maendeleo ya nchi yake?

Ni wazi, bila uzalendo maendeleo ni muhali. Tutabaki kuwavutia wawekezaji wa kuja na kusomba utajiri wetu kwa thamani ya matrilioni tukiwa tumewahakikishia usalama kwa lugha yetu maarufu ya “amani na utulivu” tunayotamba nayo duniani kote, huku sisi tukipanga Bajeti zetu kwa kuziangalia sigara, bia na soda kama vyanzo  vikuu vya mapato yetu!

Nimalizie kwa kusema kwamba mimi sio mchumi, wala sio taahira. Ningeomba wanaojiita wachumi wanieleze kwa lugha nyepesi namna tunavyoweza kujihakikishia pato la nchi kwa kuvikomalia tu vitu vinavyouzwa kwa shilingi 100 – 2000, tukiwa tumevipa kisogo vyenye thamani ya matrilioni ya shilingi!


0784 989 512
Next Post Previous Post
Bukobawadau