Bukobawadau

MISS HONDURAS 2014 AKUTWA AMEKUFA

Tegucigalpa, Honduras. Polisi wa Honduras wamesema wamepata miili inayodhaniwa kuwa ya mrembo wa nchi hiyo aliyepotea siku sita zilizopita pamoja na dada yake.
Mkuu wa Polisi, Jenerali Ramon Sabillon alisema jana kuwa wanasubiri taarifa rasmi za uchunguzi wa kitaalamu kwenye mwili unaodhaniwa kuwa wa Maria Jose Alvarado, 19 na dada yake, Sofia, 23.
Alisema jana kuwa rafiki wa kiume wa Sofia,  Plutarco Ruiz,  na rafiki yake, Aris Maldonado walitiwa mbaroni.
Mrembo huyo alitarajiwa kuondoka Jumapili kwenda London, Uingereza kushiriki mashindano ya urembo ya dunia, Miss World 2014. Mamlaka za umma nchini Honduras zimethibitisha kushikiliwa kwa watu wanne wakihojiwa kutokana na kutoweka kwa mrembo huyo. Mbali ya rafiki wa kiume wa Sofia, mtu mwingine anayeshikiliwa ni mmiliki wa eneo la biashara ambako wanadada hao walitoweka, alieleza msemaji wa Polisi, Luteni Joseph Coello, ingawa hakuwa tayari kutoa maelezo zaidi. “Kimsingi, tuliwakamata watu kumi, lakini sita kati ya hao tuliwaachia,” alieleza Luteni Coello.
Kwa mara ya mwisho, Maria na dada yake, Sofia walionekana Alhamisi kwenye eneo la Santa Barbara,  maili  240 magharibi mwa Tegucigalpa,ambako walikwenda kwa sherehe ya kuzaliwa za Ruiz.
“Mashuhuda walieleza kuwa binti yangu aliondoka akiwa na wanaume watatu,” alieleza mama mzazi, Teresa Munoz. “Nilijaribu usiku mzima kuwapigia simu zao, lakini hazikujibiwa.”
Kulingana na Umoja wa Mataifa (UN), Honduras ina matukio kiwango kikubwa cha mauaji mengi. Mengi yanahusishwa na biashara ya dawa za kulevya, rushwa.
Next Post Previous Post
Bukobawadau