Richmond iliondoka na Lowassa Escrow itamuachaje Pinda?
Na
Prudence Karugendo
SAKATA
la wizi wa pesa za Akaunti ya Tegeta Escrow limefumua mambo mbalimbali na
kuyaweka wazi pasipo wahusika kujua kuwa wanachokifanya kinatoa picha tofauti
na waliyoikusudia.
Mojawapo
ya vitu vilivyojiweka wazi ni kwamba nchi imeonyesha namna inavyoendeshwa
kiuigizaji. Hiyo ni kutokana na mambo yanayoonyesha ni ya muhimu, na
yanayotakiwa kuwa muhimu kweli kwa uendeshaji wa nchi kutotiliwa maanani
wala kuzingatiwa.
Mfano,
nchi inaye Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), huyu
anatambuliwa kikatiba na kisheria. Anachokiona na kukisema kwa upande huo
kinatakiwa kiheshimiwe na kuzingatiwa. Vinginevyo nchi inaweza kujikuta
imeangukia kwenye usemi wa “mali bila daftari hupotea bila habari”.
Lakini,
kimaigizo, ripoti zake zinaonekana zimeanza kudhalilishwa na kukebehiwa
na baadhi ya watu wasio na taaluma katika fani hiyo ya udhibi na ukaguzi! Na
hata kama wanayo taaluma hiyo lakini hawako kwenye nafasi ya kuionyesha dhidi
ya alichokifanya yeye CAG, kwa vile kimamlaka hawana sifa hiyo.
Mkaguzi na
Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali kafanya ukaguzi na kugundua kwamba pesa ya
Akaunti ya Tegeta Escrow ni mali ya umma, akaonyesha kwamba pesa hiyo imechotwa
kifisadi kwa njia za wizi na watu wanaojifanya kuwa pesa hiyo ni ya kwao.
Katika
hilo naamini kabisa kwamba hakuna mtu mwingine wa kutuambia vinginevyo. Sababu
aliyewekwa kikatiba kushughulikia suala hilo ni CAG, na si mwingine.
Kama hilo
tunalitilia shaka ina maana gani ya kuendelea kuwa na nafasi hiyo ya CAG ambayo
tunailipia kwa pesa za kodi zetu?
Sasa
anapotokea profesa wa miamba, Sospeter Muhongo, tena aliyelazimisha ukaguzi wa
CAG kufanyika kwenye eneo analoliongoza kutokana na utendaji wake wenye
mashaka, akasema ripoti ya CAG siyo sahihi anadhamiria kuonyesha kitu gani?
Kama profesa huyo haonyeshi kwamba nchi inaendeshwa kimaigizo ni kitu gani
anatuonyesha?
Muhongo ni
profesa wa miamba na Waziri wa Nishati na Madini, CAG ni mtaalamu wa ukaguzi na
mahesabu na ni Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabau za Serikali, fani na
nyadhifa mbili tofauti kabisa. Kama CAG angekuwa mwalimu kama
Muhongo bilashaka naye angekuwa profesa katika fani yake kama alivyo Muhongo.
Kwahiyo kwa nini neno profesa linamtia Muhongo kiburi na jeuri kiasi cha
kuziona taaluma na nyadhifa nyingine ni za ovyo na ana uwezo wa kuziingilia
namna atakavyo yeye?
Suala
lililopo kwa sasa ni wizi wa pesa za umma. Muhongo anaonekana kuubariki wizi
huo kwa madai ya kwamba pesa hizo siyo za umma, lakini ukaguzi umefanyika na
kubainisha kuwa pesa hizo ni za umma. Hatahivyo Muhongo bado anasisitiza kuwa
sio pesa za umma!
Tumueleweje
Muhongo? Au kwa vile ni profesa hataki kukaguliwa kama utaratibu ulivyo?
Uprofesa wa miamba unamfanya azidharau taaluma za watu wengine! Hili lingekuwa
ni suala linalohusiana na miamba nisingekuwa namshangaa hata kidogo, sababu
angekuwa yuko jikoni kwake. Lakini sivyo ilivyo, hili ni suala la mahesabu na
wataalamu wa kazi hiyo wapo.
Maigizo
mengine yamejionyesha kwa baadhi ya wabunge kuikebehi ripoti na maoni ya PAC
chini ya uenyekiti wa Zitto Kabwe. Hiki ni chombo cha Bunge ambacho kinapaswa
kuakisi mwonekano wa Bunge zima. Sasa wanapotokea baadhi ya wabunge wakaonekana
wanakinzana nacho tuwaeleweje? Ina maana hao wana Bunge lao tofauti na hili la
kwetu au wanataka tu kutuaminisha kuwa wanafanya maigizo?
Ikumbukwe
kwamba Kamati hiyo ya PAC ndiyo inayochunguza na kutoa maamuzi kwa niaba ya
Bunge kwa upande wa Hesabu za Seerikali.
Katika
suala hili la Tegeta Escrow Account Kamati hiyo haikutoa mapendekezo yake
kulingana na inavyopendelea yenyewe, isipokuwa mapendekezo yake yametokana na
ripoti ya CAG ambayo imechambua ukweli na kuuweka wazi.
Ni ripoti
hiyo iliyoifanya PAC ipendekeze ni nini cha kufanya kufuatia ukweli huo
ulioonyeshwa na CAG. Lakini sio lazima mapendekezo ya PAC yafanane na ya CAG
neno kwa neno. Sababu CAG katoa ripoti ya ukaguzi wa alichokigundua na kukiona
na baadaye kulikabithi Bunge. Bunge nalo kupitia kwenye Kamati yake ya kudumu
(PAC) likatoa hukumu. Baada ya hapo kilichoendelea ni kama maigizo ya kutaka
kuipindua hukumu hiyo, yaani kulivua Bunge dhima yake ya kuisimamia serikali.
Kingine
kinachodhihirisha maigizo yanayofanyika Bungeni ni baadhi ya wabunge kuchangia
kwenye suala la wizi wa pesa za “Tegeta Escrow Account” bila kukielewa
wanachokichangia. Sababu wapo wanaouliza ni sababu gani PAC imependekeza
waziri mkuu, Mizengo Pinda, awajibike. Hao wanaoonyesha kwamba nafasi ya waziri
mkuu inamfanya aliyeikalia abaki kama sanamu tu lisiloweza kuhangaika
kushughulikia yaliyo chini yake!
Nadhani
kumtetea waziri mkuu kwa namna hiyo ni kumtukana na kumdhalilisha, waziri mkuu
sio sanamu. Yeye ni msimamizi wa shughuli za kila siku za serikali. Kwahiyo
hakuna namna yoyote ambayo madudu ya kuwaumiza wananchi yanaweza yakafanyika
ndani ya serikali yeye akaruka kwa madai ya kwamba hayatambui wala hahusiki.
Mambo yote
yanayofanyika chini yake, awe anayajua au hayajui, moja kwa moja yanamgusa yeye
na ndiye mwenye kuwajibika. Huo ndio usimamizi kwa maana halisi, vinginevyo
hatuna sababu ya kuwa na nafasi hiyo ya waziri mkuu.
Ikumbukwe
waziri mkuu aliyemtangulia Pinda, Edward Lowassa, aliwajibika katika mazingira
yanayofanana fanana na haya aliyomo waziri mkuu wa sasa, Pinda. Sasa kama
mazingira ni yaleyale, inawezekanaje yawe haramu kwa Lowassa lakini kwa Pinda
yawe halali?
Hatahivyo
ukubwa wa kashfa iliyomfanya Lowassa kuwajibika, kimuonekano, haufikii hata
nusu ya ukubwa wa kashfa ambayo Pinda kang’ang’ana nayo na kuona kuwajibika ni
kitu ambacho hakiwezekani kwake! Hilo linathibitishwa na yaliyotokea Bungeni
ambapo kikao cha Bunge kimevunja rekodi tangu nchi yetu ijitawale, ya
kuendeshwa hadi saa tano usiku suala likiwa, pamoja na mambo mengine, kujaribu
kumnusuru waziri mkuu asiwajike.
Suala la
waziri mkuu kuwajibika inabidi tulitazame kwa kuziangalia nchi kama India,
Japan na nyingine za aina hiyo ambako jambo la waziri mkuu kuwajibika kwa kujiuzulu,
hata kama ni baada ya kukaa madarakani kwa wiki moja tu kutokana na mambo
kwenda mrama chini yake, ni jambo la kawaida kabisa.
Bilashaka
hiyo ni moja ya mambo yanayozifanya nchi hizo ziwe mbele yetu kwa mbali
kiuchumi. Lakini sisi tunamng’ang’ania waziri mkuu ambaye kila kukicha
kunatokea madudu chini yake yenye muonekano wa kuuteketeza uchumi wa nchi na
kuwatia wananchi mashakani! Hiyo nini maana yake? Tuseme kwamba tunaupenda sana
ufukara?
Kwa
vyovyote vile Pinda anapaswa awajibike kama kweli anaipenda nchi yake na
kuwathamini wananchi wenzake. Mbali na hiyo itaonekana hata uwaziri mkuu wa
Pinda nacho ni cheo cha maigizo kama niliyoyataja hapo juu. Sababu cheo chenye
dhamana ya kuwatumikia wananchi kisicho na kuwajibika hakionyeshi kinawezaje kuwahakikishia
wananchi kuwa kina manufaa kwao. Mtu ambaye hayuko tayari kuwajibika kwa
vyovyote vile hawezi kuwahakikishia wananchi kuwa atawalinda.
0784
989 512