Bukobawadau

SALMIN NA DEKO LA KISIASA ZANZIBAR

NA PRUDENCE KARUGENDO
INASHANGAZA  kwamba mpaka sasa bado kuna watu wanaoendekeza deko la kisiasa katika bara la Afrika wakati huu wa karne ya kistaarabu! Deko linalotokana na mtu kuzitegemea nguvu za dola alizozishikilia na kuzichukulia kama mhimili pekee wa kisiasa badala ya kuwategemea wananchi ambao ndio wanaopaswa kutoa maamuzi ya mwisho kwa nchi yao kwa vile ndio wenye nchi, nchi ni mali yao.
Deko la aina hiyo limeshuhudiwa sana, hasa katika bara la Afrika, katika karne iliyopita, ambapo watu walifikia kujipachika urais wa maisha kana kwamba wangeishi milele! Hiyo yote ni kwa sababu ya deko la kisasa. Katika kuendeleza deko hilo wamefanya mengi kama kutesa na hata kuua.
Lakini baada ya mtikisiko wa kisiasa uliolikumba bara la Afrika katika karne hii tuliyomo, mtikisiko ambao umedhihirisha kuwa wananchi ndio wenye nguvu za mwisho katika nchi zao, nguvu ya umma, nilitegemea kwamba deko la baadhi ya wanasiasa lingepungua na hata  kuisha kabisa.
Mfano, tumeyasikia yaliyotokea majuzi kule Burkina Faso. Rais Blaise Compaore aliyedeka kwa karibu miaka 27 akiiona nchi hiyo kama mali yake binafsi, alitimuliwa na wananchi kama mbwa koko baada ya kutaka kulifanya deko lake liwe la kudumu maisha yake yote,  wananchi wakasema hapana inatosha.
Kwahiyo nilidhani hilo la Compaore lingekuwa fundisho zuri kwa watawala wa Afrika walio na vimelea kama vya kwake, nilikuwa na imani hiyo kutokana na tukio lenyewe kuwa la hivi karibuni. Ila kulingana na ubaya wa deko la kisiasa ulivyo inaonekana watawala wengi wa Afrika hawakulitilia maanani tukio hilo!
Niseme kwamba deko ni mbaya kuliko hata ujambazi. Mtoto aliyedekezwa ni hatari kwa familia yake kuliko mtoto mwenye tabia ya ujambazi. Madhara ya ujambazi mara nyingi yanampata tu anayejihusisha na ujambazi, lakini madhara ya deko yanaweza hata yakaiteketeza familia nzima, baba mama na watoto wenzake na mwenye deko. Deko ni hatari sana.
Mfano kule Zanzibar madhara ya deko la kisiasa yameanza kujionyesha baada ya Mnadhimu wa Baraza la Wawakilishi, Salmin Awadhi Salmin, kutamka kwamba wananchi watapiga kura hadi vidole vikatike lakini hawatabadilisha  chochote katika Ikulu ya nchi hiyo! Deko la ajabu. Kawaida mwenye deko haangalii uwezo wa watu wengine.
Salmin anadai kwamba Ikulu ya Zanzibar ilipatikana kwa njia ya mapinduzi baada ya kuondolewa kwa utawala wa kisultan mwaka 1964. Eti hiyo ni baada ya njia ya demokrasia kukwama tangu mwaka 1957.
Kwa deko linalomfanya aonekane kama mlevi, Salmin amediriki kutamka kwamba hata umoja wa kitaifa Zanzibar,  unaoufanya upinzani na chama tawala vishirikiane katika kuiongoza nchi, ni bora uvunjike. Hiyo haina tofauti na mtoto mwenye deko anavyoweza kuchezea moto kijeuri na kusababisha nyumba iungue na kuteketeza familia nzima.
Maneno hayo ya deko lililojaa hatari tupu, Salmin kayasemea kwenye mkutano wa kupokea kinachoitwa Katiba Mpya inayopendekezwa katika uwanja wa Jitimahi, mkoa wa Mjini Magharibi, Unguja.
Bila deko ingembidi Salmin ajiulize maana ya mapinduzi ni nini. Sababu mapinduzi sio tu kuipata Ikulu kwa maana ya kuuondoa mfumo batili unaoitawala nchi na kuingiza mfumo mwingine batili. Mapinduzi yanalenga kuondoa utawala kandamizi kwa wananchi na kuweiweka nchi mikononi mwa wananchi ili wakaamue wenyewe wanataka nchi yao iendeshweje.
Lakini kauli ya Salmin ya kwamba wapinzani hawataiona Ikulu kamwe inaonyesha kwamba uliondolewa usultan ukarudishwa usultan mwingine, kitu ambacho ni sawa na kazi bure.
Sio kwamba Wazanzibari walimchukia sultan kwa sababu ya rangi yake ya Kiarabu, hapana, waliuchukia usultan kwa vile hawakushirikishwa kumpata sultan. Na baada ya hapo utawala wa sultan ulitaka mfumo batili wa kiutawala uendeshwe kadri ya wachache walivyotaka badala ya wananchi walio wengi. Matokeo yake ni mapinduzi ambayo nina imani Salmin hakuyashiriki.
Ikumbukwe mwongozaji wa mapinduzi hayo alikuwa raia wa Uganda, John Okello, ambaye  alifanyiwa mizengwe na kutelekezwa,  kwa sababu ya kumhofia,  bila shukurani yoyote.
Sasa kama kilichofanya mapinduzi hayo yakatokea, kuwapora wananchi haki yao ya maamuzi, ndicho anachokitetea Salmin kwamba kiendelee kuwepo,  maana ya mapinduzi ni nini? Au maana yake ni kumuondoa sultan mwarabu na kumuweka sultan mweusi?
Ikumbukwe kwamba sio Zanzibar peke yake iliyofanya mapinduzi ya kuyaondoa maamuzi kwa wachache na kuyaweka mikononi mwa wananchi walio wengi. Nchi nyingi duniani zimefanya hivyo. Nitoe mfano mmojawapo wa nchi ya Ufaransa. Mapinduzi yaliyofanyika katika nchi hiyo kati ya mwaka 1789 – 1799, yalilenga kuuondoa utawala wa kifalme, sawa na usultan, na kuyaweka maamuzi mikononi mwa wananchi.
Kwa maana nyingine neno maamuzi ndilo tunaloliita demokrasia. Kwa sasa Ufaransa ni nchi yenye demokrasia nzuri sana duniani, hayo yakiwa ni matunda ya mapinduzi hayo yanayotajwa. Haijawahi kutokea ikasemwa kwamba maadamu Ikulu ya nchi hiyo ilipatikana kwa mapinduzi basi hakuna mwingine anayepaswa kuingia bila mapinduzi. Wananchi walifanya mapinduzi ikaisha , kwahiyo wakabaki wao na vizazi vilivyofuatia kuyafaidi mapinduzi hayo kwa kuwa na maamuzi ya ni nani aingie katika Ikulu ya nchi yao.
Lakini anayesema kwamba wapinzani hawawezi kuingia Ikulu kwa vile jengo hilo lililo makao ya mkuu wa nchi lilipatikana kwa mapinduzi, anayasema hayo kwa kusukumwa na deko la kisiasa. Sababu sio wote waliomo kwenye jengo hilo waliyashiriki mapinduzi ya Zanzibar  yaliyolifanya likawa mikononi mwa wananchi. Na wala haina maana kwamba watu wote walio kwenye upinzani hawakuyashiriki wala kuyapenda mapinduzi hayo.
Wapo wapinzani walioshiriki kwenye Mapinduzi ya Zanzibar. Na kilichowafanya wakashiriki mapinduzi hayo ndicho hiki ambacho Salmin anaapa kuwa hawatakaa wakione, demokrasia au maamuzi ya wananchi. Kwahiyo kwa kauli yake Salmin tunaweza kukubaliana naye kuwa anayaelewa mapinduzi?  Au kwa kutokujua anajikuta akifanya kazi kama wakala wa sultan?
Bila kuuliza wala kujifunza ni kwamba kauli kama ya Salmin ndiyo iliyokuwa kaulimbiu ya utawala wa kisultan. Kwa vile sultan hakuchaguliwa na wananchi basi mtu mwingine waliyempenda wananchi kuiona Ikulu zilikuwa ni ndoto za mchana. Hayo ndiyo anayoyasema Salmin Awadhi Salmin kwa sasa.
Lugha kama hizo, lugha zinazoyapora mamlaka na haki za wananchi ndizo huziingiza nchi kwenye majanga na hata ya kumwaga damu. Kama yalivyokuwa mapinduzi, damu ilimwagika sana. Kwa maana ya kauli za Salmin ni kwamba ili wapinzani waipate Ikulu ni lazima nao wamwage damu?
Kama hiyo ni tofauti na anavyofikiria yeye, ana maana gani kwamba wapinzani hawataiona Ikulu? Na kama anaelewa na kuamini kwamba CCM iko Ikulu kwa ridhaa ya wananchi anawezaje kusema kwamba wapinzani wa Zanzibar  hawataiona Ikulu milele yote? Au anataka kutuonyesha kwamba CCM haiko Ikulu kwa ridhaa ya wananchi?
Sababu wanaoamua nani aingie Ikulu na nani asiingie ni wananchi na wala sio CCM yenyewe. Sasa Salmin anawezaje kutuhakikishia kwamba yumo kwenye roho ya kila mwananchi na hivyo kuona kwamba wananchi hawawezi kukiingiza chama kingine Ikulu zaidi ya CCM?
Kitu kingine ni kwamba kwa mtu anayewatakia mema Wazanzibari hawezi kutamka maneno ya kwamba umoja wa kitaifa uliopo kwa sasa ni bora uvunjike. Ubinafsi pekee ndio unaoweza kumsukuma mtu kutoa kauli ya aina hiyo. Hiyo ni kauli iliyojaa maslahi binafsi, isiyowajali Wazanzibari wengine.
Nimalizie kwa kusema kwamba deko la kisiasa ni kitu hatari sana. Sababu anayeendekeza deko la aina hiyo hawezi kuufikiria mustakabali wa nchi wala wa wananchi hata mara moja, yeye anachong’ang’ana nacho ni atapata ni nini binafsi kupitia timu iliyo Ikulu bila kujali majaaliwa ya nchi yake wala ya wananchi wenzake. Deko la kisiasa ni sumu,  wananchi tujihadhari nalo.
0784 989 512
Next Post Previous Post
Bukobawadau