Bukobawadau

TOFAUTI YA MUZIKI NA MAKELELE

 Tusifanye muziki na makelele kuwa ni kitu kilekile
 NA PRUDENCE KARUGENDO
KUPUNGUA  kwa vipaji vya muziki hapa nchini kwa kiasi kikubwa kumelifanya neno muziki kubadilishwa maana yake. Baada ya wanamuziki, kwa maana ya wapiga muziki, kupungua karibu na kuisha wapenda muziki wameanza kubuni njia nyingine za kuutambua muziki ilmradi neno muziki liendelee kuwepo. Katika kufanya hivyo chochote chenye kutoa sauti kinadaiwa ni muziki pasipo kutofautisha kipi ni muziki na kipi ni kelele.
 Muziki,  kwa maana halisi, ni mpangilio maalumu wa sauti zinazotoka kwenye ala, vyombo vya muziki, zinazopigwa kiufundi. Sauti inayopatikana toka kwenye vyombo hivyo ndiyo huitwa muziki.
  
Sio lazima sauti hizo ziambatane na maneno, hata kama maneno yanaingizwa, nyimbo, ni kwa ajili tu ya kuurembesha muziki, sababu maneno peke yake hayawi muziki bali ni nyimbo. Bado muziki unabaki kuwa sauti zinazotokana na vyombo vinavyochezwa na binadamu.
 
Hiyo ndiyo sababu kikundi cha watu, kwaya kwa mfano, kinachoimba bila kucheza vyombo vya muziki hakiitwi kikundi cha wanamuziki bali kikundi cha nyimbo au cha waimbaji. Vivyo hivyo kwa waimbaji wa mashairi, hawaitwi wanamuziki, ni kwa sababu mashairi mara zote hayahusishi vyomvo vya muziki.
 Lakini kwa watu wenye kutumia vyombo vya muziki kutoa sauti, hata kama hawaweki maneno ya nyimbo, kama zilivyo bendi za Polisi na Jeshi zitumbuizapo kwenye shughuli maalumu kama gwaride, wanaitwa wanamuziki kutokana na uwezo wao wa kucheza vyombo vinavyotoa muziki.
 
Sasa kutokana na ukosefu wa watu wenye uwezo kuchezesha vyombo vya muziki huku uraiani, ndipo tunaposikia kitu kinachoitwa muziki wa kizazi kipya! Hicho ni kitu wanachokifanya vijana wasio na uwezo wa kupiga muziki bali vipaji vya kutunga mashairi na kuyapeleka kwa watu wanaoitwa maprodyusa, hao kazi yao ni kuwatafutia midundo iliyotengenezwa kwenye kompyuta na kuichanganya na mashairi yao, baadaye unakuwa muziki wa kizazi kipya!
 Kusema ukweli hapo hakuna muziki, ni makelele tu. Sababu muziki unatengenezwa na ala za muziki na si vinginevyo. Au kama ni hivyo basi kompyuta ndiyo tunaweza kuiita mwanamuziki kwa vile ndiyo inayotoa midundo hiyo. Lakini sio yule aliyepeleka mashairi yake ili akatafutiwe midundo.
Isipokuwa midundo hiyo kuiita muziki ni kwakuwa muziki wenyewe unaelekea kutoweka siku hizi. Kwahiyo kwa kujifariji ili iendelee kuonekana muziki bado upo ndipo yanapotajwa mambo kama ya muziki wa kizazi kipya. Ni kujifariji tu.
 
Mtu anayeshiriki kutengeneza muziki, hata kama ni mwimbaji tu asiyejua kucheza chombo chochote cha muziki kama gitaa, kupuliza saksafoni, ngoma nakadhalika,  anaitwa mwanamuziki sababu ana utaalamu wa kupanga sauti ya maneno ya wimbo ili yaendane na midundo ya muziki.
Kituko ni pale mtunzi wa mashairi asiyejua hata sauti inayofaa kuimbia mashairi yake mpaka atafutiwe na prodyusa, mbali na kutoweza kupiga chombo chochote cha muziki, eti naye anataka aitwe mwanamuziki! Kwa muziki gani?
 
Nashangaa vijana wengi kwa sasa wanaoimba nyimbo zinazoitwa muziki wa kizazi kipya wanaitwa wanamuziki! Sielewi ni kitu gani kinachofanya waitwe wanamuziki wakati kusema ukweli kwenye nyimbo zao, au niyaite mashairi yao, hakuna muziki wowote unaochezwa mle. Kwa nini tunalazimika kulidhalilisha neno muziki?
 
Kinachoonyesha kwamba wanachokifanya vijana hawa wa siku hizi ni tofauti kabisa na muziki, ni pale wanapoitwa kupiga muziki wa moja kwa moja “live concert”. Badala ya kujiandaa na vyombo vya muziki wao wanatayarisha vyombo vya disco, muziki wa kunukuu ambao mara nyingi unakuwa umerekodiwa  kwenye vyombo viitwavyo CD siku hizi,  mpaka wanamuweka na DJ!
 
Wakati wa kuimba mwimbaji anasema awekewe CD fulani naye kuanza kufanya maigizo kama anaimba vile kumbe sauti inayosikika inatoka kwenye CD kwa mtindo huitwao “play back”. Kweli hapo kuna live concert?
 
Kwakeli tunapaswa kutofautisha muziki na kelele, kwa maana sio kila kelele tuzisikiazo ni muziki. Vinginevyo kwa mtindo huo hata mingurumo ya radi wakati wa mvua itabidi tuicheze kwa kujiridhisha kuwa ni muziki wa asili tuliotengenezewa na Mungu.
 
Hata mingurumo ya mabomu yaliyojilipua Mbagala na Gongolamboto tungeicheza kwa kuamini kuwa ni muziki. Kama sio hivyo basi tuelewe kwamba muziki na kelele ni vitu viwili tofauti.
Kinachofanyika kwa wakati huu na kupewa jina la muziki wa kizazi kipya kwa kiasi kikubwa ni makelele. Hilo jina la kizazi kipya ni la kujifariji kutokana na kutokuwepo kwa muziki wenyewe. Huwezi kuwa na muziki hai bila vyombo vya muziki.
 
Kuna usemi katika lugha ya Kihaya usemao kwamba “obworo bushomba obumaza” ukiwa na maana ya kwamba ukosefu wa kitu, umasikini, hushawishi ujasiri. Ndio kama ujasiri huo wa kudai makelele yanayofanywa na fijana kwa sasa ni muziki wa kizazi kipya! Tutafanyaje kama muziki haupo?
 
Na tatizo hili naona halipo tu hapa kwetu, limetamalaki hata kwenye nchi nyingine. Ndiyo maana nimesikia kijana mmoja wa Kitanzania anayejulikana kama Diamond akipewa tuzo kedekede za kimataifa eti ni mwanamuziki bora wakati hana uwezo wowote wa kupiga muziki isipokuwa kuimba tu mashairi.
 
Kama tuzo hizo alizopewa zisingehusishwa na muziki ningempongeza sana Diamond, lakini kwa sasa inaniwia vigumu kumpongeza kwa kitu ninachoamini kwamba hakijui hata kidogo. Kweli “obworo bushomba obumaza”. Lakini mimi sitaki tufike huko.
Tuwashauri vijana wa kisasa wajifunze kupiga muziki kama wanahitaji kuitwa wanamuziki kusudi tunapowakaribisha kupiga muziki hai, “live concert” watupigie muziki wa kweli unaotoka kwenye ala za muziki na sio kutuwekea CD zinazotoa sauti zilizotengenezewa kwenye kompyuta huku wenyewe wakifanya maigizo wakati hawaimbi.
Ningewashauri vijana hawa wa kinachoitwa Bongo Fleva wakajifunze muziki kwa kijana aitwaye Banana Zorro au kwa Judith Wambura (Lady Jaydee) namna ya kupiga muziki na kuacha kutuzuga na makelele wakidai ni muziki wa kizazi kipya au Bongo Fleva.
 Hebu tulipe neno muziki hadhi yake kwa kuucheza muziki wenyewe na kuacha kufanya vituko kutokana na kuishiwa.
 
0784 989 512
Next Post Previous Post
Bukobawadau