Bukobawadau

UTETEZI WA GURUMO WA IKULU WAZUA MSHANGAO


MAJIBU tata ya Mnikulu, Shabani Gurumo mbele ya Baraza la Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma yalizua mshangao kwa wananchi waliokuwepo.
Pia utetezi huo ulizua mvutano mkubwa kati ya Gurumo na wanasheria wa sekretarieti ya maadili, kwa upande mmoja, na pia mvutano kati ya wanasheria hawa na wakili wa Gurumo, kwa upande mwingine.
Mwansheria: Majina yako kamili ni yapi kiongozi?
Gurumo: Naitwa Shaban Rajab Gurumo.
Mwanasheria: Kiongozi, unaweza ukaliambia Baraza hili unafanya kazi gani?
Gurumo: Kazi yangu ni mnikulu. Nasimamia watumishi wote wa ndani ya Ikulu; nasimamia ukarabati wa majengo yote ya Ikulu; naratibu ikulu ndogo zote nchini; napokea mabalozi wapya kutoka nchi za nje; na ninaandaa tafrija zote za ikulu zinazomhusisha rais.
Mwansheria: Kiongozi, akaunti namba 00110102645401 iliyofunguliwa Benki ya Mkombozi 04 Februari mwaka 2014 ni ya nani?
Gurumo: Akaunti hiyo ni yangu. Niliifungua baada ya rafiki yangu James Rugemalira kunielekeza nifungue akaunti katika benki hiyo?
Mwansheria: Kiongozi, tarehe 05 Februari 2014 akaunti hiyo ilipokea shilingi 80,850,000. Hiyo fedha ni mali ya nani?
Gurumo: Hiyo fedha ni mali yangu halali.
Mwansheria: Kiongozi, hiyo fedha ulipewa na nani?
Gurumo: Nilipewa na rafiki yangu aitwaye James Rugemalira.
Mwanasheria: Kiongozi, wewe na James Rugemalira mlifahamiana vipi na tangu lini?
Gurumo: Sikumbuki vizuri. Lakini nadhani nilimfahamu tangu zamani kupitia daktari wa familia yangu aitwaye Fred Limbanga, ambaye nimekuja naye hapa leo kama shahidi. 
Mwansheria: Kiongozi,  kwenye nakala ya Ankara za benki uliyowasilisha katika ofisi za sekretarieti ya maadili inaonekana fedha hizo zilitoka kampuni ya VIP Engineering and Marketing Ltd na sio kwa James Rugemalira. Unasemaje kuhusu jambo hili?
Gurumo: (Anatazama nakala ya ankara kwanza). Ndio leo nimeligundua jambo hili. Hapo kabla sikuwa nimechukua muda kuisoma ankara hii. Muda wote nilijua fedha zimetoka kwa James Rugemalira.  
Mwansheria: Kiongozi, hiyo fedha ulipewa kwa ajili gani na ziliambatana na masharti gani?
Gurumo: Sikuambiwa ni kwa sababu gani na hakuna masharti yoyote niliyopewa kuhusu matumizi yake. Naomba akaulizwe James Rugemalira.
Mwanasheria: Kiongozi, James Rugemalira alikuingizia fedha hizo kwa sababu uliziomba au hapana?
Gurumo: Sikumwomba James Rugemalira fedha. Na sijui kwa nini aliniwekea fedha hizo. Hata aliponiambia nifungue akaunti benki ya Mkombozi ili aniwekee fedha sikumwuliza fedha hizo ni za nini. (Kicheko kutoka kwa wananchi).
Mwansheria: Kiongozi, kwa sasa karibu fedha yote umekwisha kuitumia. Uliitumia katika mambo gani na kwa nini?
Gurumo: Niliitumia katika matumizi mbalimbali yakiwemo matibabu ya ugonjwa wa kansa uliokuwa unamsumbua mke wangu. 
Mwansheria: Kiongozi, fedha hizo ambazo umekiri ni mali yako, uhalali wake unatokana na nini. Ni mshahara, posho, faida katika biashara, urithi, kuokota, zawadi au kitu gani?
Gurumo: Sio mshahara, posho, faida katika biashara, urithi, au zawadi. Pia hazikuokotwa. Ni fedha nilipewa tu. (Kicheko kutoka kwa wananchi).
Mwansheria: Kiongozi, unawezaje kutumia fedha nyingi kiasi hicho bila kwanza kutafiti sababu fedha hizo kuingizwa katika akaunti yako? 
Gurumo: Sikuwa na hofu yoyote kwani James Rugemalira ni rafiki yangu kwa zaidi ya miaka kumi sasa.
Mwansheria: Kiongozi, kwa mujibu wa sheria ya maadili ya viongozi wa umma, umewahi kutoa taarifa ya fedha hizi kwenye sekretarieti ukionyesha kwamba ni miongoni mwa mali yako mpya?
Gurumo. Tayari. Nilifanya hivyo tangu 29 Desemba, 2014 kupitia fomu maalum. Fedha hizi zimetajwa kwenye ukurasa wa kumi na saba. (Anaonyesha nakala ya fomu aliyoijaza).  
Baada ya kikao, MwanaHalisi Online ilipata fursa ya kungea na wanasheria wa sekretarieti ya maadili kuhusu maana ya neno “zawadi” kwa mujibu wa sheria. Swali hilo pia nililielekeza kwa wakili wa Gurumo.
Kwa upande wake, Gurumo alisema neno hilo halina fasili rasmi katika sheria za Tanzania. Lakini, wanasheria wa shekretarieti walikuwa na maoni tofauti.
Walisema, “Gurumo amekiri kwamba fedha zile ni mali yake. Mali inaweza kupatikana kupitia mshahara, posho, biashara, urithi, kuokota, au zawadi. Gurumo amekanusha yote haya. Kwa hiyo fedha hizo anazimiliki kwa mujibu wa kanuni gani?,” walihoji.
“Fedha zile alizipokea kama zawadi na kinyume cha sheria ya maadili ya viongozi wa umma na atatiwa hatiani na Baraza,” walihitimisha.
CHANZO:  mwanahalisionline
Next Post Previous Post
Bukobawadau