Bukobawadau

WANANCHI MKOANI KAGERA WANUFAIKA NA MPANGO WA URASIMISHAJI WA RASILIMALI NA BIASHARA ZA WANYONGE KWA KUPATA HATI ZA KIMILA ILI KUKUZA UCHUMI WAO

Bi Seraphia Mgembe Mratibu wa MKURABITA Akitoa Neno Wananchi Waliokusanika
Bw. Rusibamaila Mkurugenzi MKURABITA Akisoma Hati Moja Moja Kwa Furaha Ili Wenyewe Wajongee Kuzipokea
Mkuu wa Mkoa wa Kagera Mhe. John Mongella Akikabidhi Rasmi Hati za Kimila kwa Wananchi
Wananchi Waliokusanyika Katika Ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Missenyi Kuja Kupokea Hati za Kimila Wakiimba Kwa Furaha.
Mkuu wa Mkoa wa Kagera Mhe John Mongella Akiwa na Katika Picha ya Pamoja na Wananchi Waliopokea Hati za Kimila


WANANCHI MKOANI KAGERA WANUFAIKA NA MPANGO WA URASIMISHAJI WA RASILIMALI NA BIASHARA ZA WANYONGE KWA KUPATA HATI ZA KIMILA ILI KUKUZA UCHUMI WAO

Mkoa wa Kagera umenufaika na  shughuli za Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge Tanzania MKURABITA  kwa kupima mashamba ya wakulima na wafanyabiashara na kutoa hati za kimila 1,0024 katika Halmashauri za Wilaya nne mkoani Kagera .
Katika sherehe za uzinduzi wa ugawaji wa Hati za Kimila zilizofanyika katika Halmashauri ya Wilaya ya Missenyi  Machi 10, 2015 jumla ya Hati za Kimila 565 ziligawiwa kwa wananchi ambao ni wakulima wa miwa pamoja na kilimo cha mazao mbalimbali  katika mashamba ya wakulima.
Mratibu wa MKURABITA Bi Seraphia Mgembe alisema kuwa mpango wa MKURABITA ulianzishwa Septemba 2003, utekelezaji wake ulianza Oktoba 2004 lengo likiwa ni kurasimisha ardhi ya wanyonge ili kukuza uchumi, kupunguza migogoro ya ardhi, na kuleta maendeleo kwa wananchi kupitia ardhi yao.
Bi Mgembe alisema kuwa baada ya kutumia mbinu za kitaalamu katika kurasimisha ardhi ya wananchi kukwama, MKURABITA waliamua kuzitumia Halmashauri za Wilaya ili kuwafikia wananchi kwa urahisi zaidi jambo ambalo linaonyesha matumaini kwa kuwa wananchi wana mwitikio mkubwa sana hasa mkoa wa  Kagera.
Aidha MKURABITA kupitia mpango huo wa urasimishaji wa raslimali za wanyonge hasa ardhi hutoa mafunzo  ya kuwajengea uwezo  watumishi wa Idara ya Ardhi katika Halamashauri na kuwawezesha vifaa vya kisasa vya kupimia ardhi ili zoezi la upimaji na utoaji wa hati za kimila  liwe endelevu katika Halmashauri husika.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Kagera Mhe. John Mongella aliyekabidhi hati hizo kwa wananchi 565 wa Wilaya ya  Missenyi aliwashukuru MKURABITA kutoa hati hizo kwa  wananchi wa mkoa wa Kagera a pia  alisema kuwa wananchi watazitumia hati hizo kujikomboa kiuchumi kwa kuapata mikopo toka katika taasisi za Kifedha.
 Mhe.John Mangella aliwaasa wananchi waliopata hati hizo kuzitumia kuinua uchumi wao kwa kunzia mwananchi mmoja mmoja, kaya , kitongoji hadi ngazi ya kijiji. Aidha aliwakumbusha kuwa maendeleo ili yawepo kunahitajika ardhi, watu, uongozi bora na siasa safi Kama Mwlimu  Nyerere alivyowahi kunena.
Aidha, aliwaagiza Wakurugenzi  Watendaji wa Halmashauri za Wilaya  katika mkoa wa Kagera kuendeleza zoezi la kupima mashamba ya wananchi na kila baada ya miezi mitatu watoe hati za kimila angalau 200. Vilevile waliaswa kuvitunza vifaa vya upimaji wanavyowezeshwa na MKURABITA mara baada ya kuwajengea uwezo.
Mkuu wa Mkoa Mhe. John Mongella aliziomba taasisi za Kifedha hasa benki ya Wakulima mkoani Kagera kuzitambua hati za kimila na kuwakopesha wananchi wenye hati hizo bila mizengwe kwani hati hizo zinatambuliwa na serikali kuwa ni hati halali zenye dhamana kwa mashamba ya wananchi.
Akimalizia Mkuu wa Mkoa Mhe. John Mongella alimwomba mratibu wa MKURABITA kuufanya mkoa wa Kagera kuwa ni mkoa wa mfano katika kupima mashamba ya wananchi na kutoa hati za kimila kutokana na wananchi kuonyesha mwamko mkubwa wa kupimiwa mashamba yao ili wapate hati hizo.
Naye John Rugeiyamu Mwenyekiti wa Kijiji cha Mabuye Halmashauri ya Wilaya ya Missenyi kwa niaba ya  wananchi waliopata hati za kimila alisema hati zimekuja kwa wakati muafaka kwani watazitumia kupata mikopo ya kuinua uchumi wa maisha yao na zitapunugza sana migogoro ya ardhi katika vijiji.
Meneja Msaidizi Benki ya Wakulima Bw. Nthony Nzigula alisema wananchi waliopata hati za kimila wanaruhusiwa kukopa katika benki yao ambayo kwa sasa ina mpango wa kufungua matawi yake kupitia SACCOS ambazo tayari wamezibainisha kila Wilaya ili kusogeza huduma zao karibu na wananchi.
Halmashauri za Wilaya zilizonufaika na Urasimishaji wa Raslimali za Biashara za Wanyonge Tanzania ni Muleba  hati 3271, Ngara hati 2962, Karagwe hati 3238, na Missenyi hati 565 jumla wakulima waliopata hati za kimila katika mkoa wa Kagera 10,024. Aidha mwaka wa fedha 2015/16 zoezi hilo litafanyika katika Halmashauri ya Wilaya ya Biharamulo.
Next Post Previous Post
Bukobawadau