Bukobawadau

EWURA YATANGAZA KUSHUKA KWA BEI YA MAFUTA NCHINI


Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), Felix Ngamlagosi (kulia), akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari Dar es Salaam leo, kuhusu bei kikomo za mafuta aina ya petroli kuanzia leo. Kushoto ni Mkurugenzi wa Umeme, Mhandisi Anastas Mbawala.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), Felix Ngamlagosi (katikati), akisisitiza jambo katika mkutano huo. Kushoto ni Mkurugenzi wa Umeme, Mhandisi Anastas Mbawala na kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa Petroli, Gerald Maganga.


 Mkutano na wanahabari ukiendelea.


Na Dotto Mwaibale

MAMLAKA ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imetangaza kushuka kwa bei ya mafuta nchini kuanzia kesho Machi 2, 2016.

Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari ofisini kwake Dar es Salaam leo mchana, Mkurugenzi Mkuu wa  (EWURA), Felix Ngamlagosi alisema bei ya Petroli imeshuka sh. 31 kwa lita sawa na asilimia 1.70, Dizeli sh. 114 kwa lita sawa na asilimia 7.10 na mafuta ya taa kwa sh. 234 kwa lita sawa na asilimia 13.75 ikilinganishwa na mwezi uliopita.

Alisema hapa nchini kwa sasa Petroli itauzwa Sh. 1,811, Dizeli sh. 1,486 na mafuta ya taa sh. 1,465.

Alisema kupungua kwa bei hizo kwa soko la ndani  kumetokana na kuendelea kushuka kwa bei za mafuta katika soko la dunia.

Hata hivyo alisema hakutakuwa na mabadiliko yeyote ya bei ya petroli na dizeli kwa mkoa wa Tanga kwa mwezi huu na kwamba hiyo imetokana na kutopokea mafuta mapya kupitia Bandari ya mkoa huo katika kipindi cha Februari mwaka huu.

"Mamlaka inapenda kuujulisha umma kuwa bei hizi kikomo za mafuta kwa eneo husika zinapatikana vilevile kupitia upigaji wa simu ya mkononi kwa mitandao yote kwenda  namba  *152*00# na kisha kufuata maelekezo.


Aliongeza kuwa kwa mujibu wa sheria ya mafuta ya mwaka 2015, bei za bidhaa za mafuta zitaendelea kupangwa na soko hivyo Ewura itaendelea kutoa taarifa za bei kikomi lengo likiwa ni kuwasaidia wadau kufanya maamuzi stahiki kuhusu manunuzi ya bidhaa hiyo.

Aidha amevitaka vituo vyote vya mafuta nchini na kuchapisha bei za bidhaa za mafuta katika mabango yanayonekana bayana na yakionesha bei ya mafuta, punguzo, vivutio vya biashara au promosheni zinazotolewa na kituo husika.

Alisema wateja wanashauriwa kununua bidhaa za mafuta kutoka kwenye vituo vinavyouza mafuta kwa bei ndogo zaidi ili kushamirisha ushindani. Ni kosa kuuza mafuta bila kuweka mabango ya bei inayoonekana vizuri kwa wateja na adhabu itatolewa kwa kituo husika.

Alibainisha kuwa wanunuzi wanashauriwa kuhakikisha kuwa wanapata stakabadhi ya malipo inayoonesha jina la kituo, tarehe, aina ya mafuta kwa lita na kwamba stakabadhi ya malipo itatumika kama kidhibiti cha mnunuzi wa mafuta endapo kutajitokeza malalamiko ya ama kuuziwa mafuta kwa bei ya juu kuliko bei kikomo, au yenye kiwango cha ubora kisichofaa.



Next Post Previous Post
Bukobawadau